Serikali ya Mkoa wa Mwanza imemshukuru Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uwekezaji alioufanya katika sekta ya afya hususani kitengo cha saratani katika hospitali ya rufaa ya kanda Bugando.

Hayo yamebainishwa na Mkuu wa Wilaya ya Ilemela Mhe. Amir Mkalipa kwaniaba ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza katika maadhimisho ya siku ya saratani kwa watoto duniani ambayo iliambatana na mchezo wa kirafiki wa mpira wa miguu kati ya timu RC na timu RMO.

Mhe. Mkalipa amesema Mhe. Rais ameimarisha matibabu ya saratani kwa kununua mashine kubwa kwa ajili ya mionzi, kupeleka wataalamu kusomea ubingwa na ubingwa bobezi juu ya maswala ya saratani lakini pia amejenga wodi kwa wagonjwa wa saratani na ametenga fedha kwa ajili ya dawa na vifaa tiba kwa ujumla pamoja na kuajiri watumishi wapya katika sekta ya afya.

Aidha, amewashukuru wadau wote ambao amekua kipaumbele katika kutoa misaada katika matibabu ya watoto ikiwemo bima na vifaa mbali mbali huku akiiomba jamii iendelee kuchangia katika jitihada za serikali katika matibabu ya watu wenye saratani.

Naye Mganga Mkuu Mkoa wa Mwanza Dkt. Jesca Lebba amewasisitiza wananchi kuwa na tabia ya kuangalia afya za watoto kwakua saratani nyingi za watoto hazijulikani chanzo chake lakini inapogundulika mapema inatibika na gharama zake zinakua ni nafuu.

Ameongeza kwa kuwataka wananchi kubadili mfumo wa maisha na kujenga desturi ya kufanya mazoezi, kula mlo ulio kamili, kupata chanjo ambazo zitawasaidia katika kujikinga na ugonjwa wa saratani pamoja na kupunguza matumizi ya kemikali, mionzi na vitu vingine vyote kama pombe, sigara na tumbaku ambavyo vinaweza kupelekea mtu kupata saratani.

Sambamba na hayo, Dkt. Lebba amesisitiza juu ya umuhimu wa bima ya afya kwa wote kwakuwa inarahisisha matibabu na inamfanya mwananchi apate huduma kwa uharaka na gharama nafuu zaidi.

Hata hivyo mchezo huo wa kirafiki uliochezwa katika uwanja wa Nyamagana umetamatika kwa timu RC kuibuka na ushindi wa bao 2 kwa 1 dhidi ya timu RMO.Veternas wa mwanza wamechangia vitu mbalimbali kwa ajili ya watoto wenye saratani.

Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Mkoa wa Mwanza, 2 Regional Drive
S.L.P: 119, Mwanza.
Simu: 028-2501037
Simu ya Mkononi: 028-2501037
Barua Pepe: ras@mwanza.go.tz
Hakimiliki©2018. Mkoa wa Mwanza . Haki zote zimehifadhiwa.