Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. Said Mtanda ameagiza Halmashauri ya Jiji la Mwanza kuwalipa wananchi fidia ya shilingi milioni 163 zilizobaki ili kupisha ujenzi wa mabweni katika Shule mpya ya Sekondari Kisoko.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa shule hiyo iliyopo Kata ya Luchelele, RC Mtanda amesema tayari shilingi milioni 187 zimelipwa, huku kiasi kilichobaki kikihusu wananchi 11. Amesisitiza malipo hayo yakamilike haraka ili maandalizi ya ujenzi wa mabweni yaanze bila kuchelewa.

Aidha, ameipongeza Halmashauri kwa kusimamia vyema mradi huo hadi kukamilika kwake, akiwataka viongozi kuendelea kuchapa kazi kwa bidii kwa kuwa kazi ndiyo kipimo cha uongozi bora.

RC Mtanda pia amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa shilingi milioni 584 kwa ajili ya ujenzi wa shule hiyo. Amesema miundombinu ipo tayari na walimu wameajiriwa, hivyo wazazi wahakikishe wanafunzi wote waliochaguliwa Kidato cha Kwanza wanaripoti shuleni.

Sambamba na hilo, amemtaka Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana kuhakikisha maabara angalau moja inakamilishwa ndani ya mwaka huu ili kuanza mpango wa maabara nyingine mwakani.

Kwa upande wake, Mkuu wa Shule ya Sekondari Kisoko Aloyce Bihege amesema shule imejengwa kupitia mpango wa kuboresha elimu ya sekondari (SEQUIP) kwa mwaka wa fedha 2024/2025, na ilipokea shilingi 584,280,029 tarehe 08 Oktoba 2024. Masomo yalianza rasmi tarehe 08 Julai 2025 na wanafunzi 147 (wavulana 67 na wasichana 80) kutoka Luchelele Sekondari.

Hadi tarehe 12 Februari 2026, shule ina jumla ya wanafunzi 290, wakiwemo 143 wa Kidato cha Kwanza 2026 (wavulana 71 na wasichana 72) kati ya 215 waliopangwa kujiunga mwaka huu. Ameongeza.

Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Mkoa wa Mwanza, 2 Regional Drive
S.L.P: 119, Mwanza.
Simu: 028-2501037
Simu ya Mkononi: 028-2501037
Barua Pepe: ras@mwanza.go.tz
Hakimiliki©2018. Mkoa wa Mwanza . Haki zote zimehifadhiwa.