Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. Said Mtanda amezielekeza Halmashauri zote za Mkoa huo kufanya tathmini ya kina ya changamoto na upungufu wa miundombinu katika Shule za Msingi na Sekondari ili kubaini mahitaji halisi na kuyaainisha mapema kabla ya kupatiwa fedha za utekelezaji.

RC Mtanda amesema si busara kwa changamoto za shule kusubiri kuibuliwa kwanza kupitia mitandao ya kijamii ndipo hatua zichukuliwe, badala yake tathmini ifanyike mapema ili kuzuia aibu na usumbufu kwa wanafunzi.

Ameyasema hayo alipokuwa akikagua maendeleo ya ujenzi wa maabara katika Shule ya Sekondari Masemele iliyopo Wilayani Ilemela ambapo amesema amekuwa akipokea ujumbe kutoka kwa wazazi wakilalamikia uhaba wa madawati katika baadhi ya shule za Wilaya hiyo.

“Ni aibu kubwa kuona wanafunzi wamekaa chini, halafu picha zinasambazwa mitandaoni ndipo tuanze kukimbizana kutafuta suluhu. Tusifikie huko,” amesema RC Mtanda.

Ameelekeza tathmini ifanyike kwa shule zote za msingi na sekondari ili kubaini maeneo yenye upungufu wa madawati, vyumba vya madarasa, matundu ya vyoo na miundombinu mingine muhimu, ili fedha zitakapopatikana zielekezwe moja kwa moja kwenye mahitaji hayo.

Aidha, amewataka watumishi wa sekta ya elimu kuelewa mazingira yao na kuweka vipaumbele kulingana na uhitaji mkubwa uliopo katika maeneo yao.

Katika hatua nyingine, RC Mtanda ametoa maagizo ya kukamilika kwa ujenzi wa maabara hiyo ndani ya wiki mbili, pamoja na kukamilisha uwekaji wa nishati ya umeme katika chumba kimoja cha maabara na kufunga tenki la maji ili kuwezesha matumizi bora ya miundombinu hiyo.

Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Mkoa wa Mwanza, 2 Regional Drive
S.L.P: 119, Mwanza.
Simu: 028-2501037
Simu ya Mkononi: 028-2501037
Barua Pepe: ras@mwanza.go.tz
Hakimiliki©2018. Mkoa wa Mwanza . Haki zote zimehifadhiwa.