Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. Said Mtanda amezindua mradi wa ujenzi wa nyumba ya mtumishi (2 in 1) katika Kituo cha Afya Budushi, Wilaya ya Kwimba Mradi uliotekelezwa kwa ushirikiano kati ya TASAF Awamu ya Tatu kupitia mpango wa TPRP IV na wananchi wa Kitongoji cha Mahiga, Kijiji cha Sumve.

Akizungumza mara baada ya uzinduzi huo, Mhe. Mtanda ameipongeza Serikali kwa juhudi za kuimarisha sekta ya afya mkoani Mwanza. Amesema ujenzi wa nyumba za watumishi utasaidia kuboresha mazingira ya kazi kwa wahudumu wa afya na kuongeza ufanisi wa utoaji huduma kwa wananchi.

Aidha, amewahamasisha wananchi wa Kwimba na Mkoa wa Mwanza kwa ujumla kuchangamkia mpango wa Bima ya Afya kwa Wote unaotarajiwa kuzinduliwa kimkoa Februari 20, 2026 katika Wilaya ya Misungwi. Amesema kila kaya itachangia shilingi 150,000 na kunufaika na huduma 378 za afya.

Akisoma taarifa ya mradi, Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Budushi, Dkt. Paulo Kanga amesema Halmashauri ya Wilaya ya Kwimba ilipokea fedha kwa ajili ya ujenzi wa nyumba mbili za watumishi (two in one) katika kituo hicho. Mradi huo uliibuliwa na wananchi wa Kijiji cha Sumve mwaka 2023.

Utekelezaji wa mradi ulianza Aprili 30, 2025 ukisimamiwa na Halmashauri kwa kushirikiana na Kamati ya Usimamizi wa Mradi (CMC) ya kijiji. Mradi huo ulifadhiliwa na TASAF kupitia mpango wa kupunguza umaskini awamu ya nne (TPRP IV).

Jumla ya gharama za mradi zilikuwa Sh. 205,521,170.58, ambapo TASAF-OPEC ilitoa Sh. 184,821,428.58 na jamii ilichangia Sh. 20,699,742.00 kupitia vifaa vya ujenzi vinavyopatikana eneo husika na nguvu kazi ikiwemo usafirishaji wa maji, mchanga, kokoto, mawe na umwagiliaji maji wakati wa ujenzi.

Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Mkoa wa Mwanza, 2 Regional Drive
S.L.P: 119, Mwanza.
Simu: 028-2501037
Simu ya Mkononi: 028-2501037
Barua Pepe: ras@mwanza.go.tz
Hakimiliki©2018. Mkoa wa Mwanza . Haki zote zimehifadhiwa.