Katibu Tawala Mkoa wa Mwanza Bw. Balandya Elikana leo tarehe 16 Februari, 2026 amepokea ugeni kutoka Wizara ya Afya, Wizara zingine na taasisi za kisekta waliofika mkoani humo kwa ajili ya maandalizi ya uzinduzi wa wodi ya kisasa ya watoto wachanga iliyojengwa wilayani Kwimba utakaofanyika hivi karibuni.

Akiongea na timu hiyo Bwana Balandya ameishukuru Wizara ya Afya kwa kushirikiana na taasisi ya Doris Mollel kupitia mradi wa Keep a Child Alive kuwezesha kukamilika kwa wodi hiyo ya viwango vya kimataifa kwani itasaidia kuimarisha huduma za watoto wachanga.

Amesema serikali imeendelea kuboreaha huduma za afya mkoani humo katika kila eneo kuanzia madawa na vifaa tiba hivyo ujio wa washirika hao ni uungaji mkono wenye tija sana kwa taifa kwani unakusaidia kuondoa vifo vya watoto wachanga vitokanavyo na uzazi na hata baada ya kuzaliwa.

Naye, Mkurugenzi wa Afya ya Uzazi, Mama na Mtoto kutoka wizara ya Afya Dkt. Felix Bundala amesema Wizara imemuomba Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kufungua rasmi wodi hiyo mnamo tarehe 01 Machi, 2026 ambapo anatarajiwa pia kuhudhuria Mkurugenzi wa WHO.

Aidha, amefafanua kuwa ujio wao Mkoani Mwanza kwa sasa ni kwa ajili ya wadau wote kuona kwa pamoja namna mradi ulivyotekelezwa na kupitishana katika namna gani jengo hilo pamoja na miundombinu yake itatoa huduma.

Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Mkoa wa Mwanza, 2 Regional Drive
S.L.P: 119, Mwanza.
Simu: 028-2501037
Simu ya Mkononi: 028-2501037
Barua Pepe: ras@mwanza.go.tz
Hakimiliki©2018. Mkoa wa Mwanza . Haki zote zimehifadhiwa.