Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. Said Mtanda amesisitiza kuwa maendeleo ya zao la choroko yanahitaji mshikamano na ushirikiano wa karibu kati ya Serikali, wakulima, sekta binafsi na wadau wa maendeleo.

Mhe. Mtanda amesema kupitia ushirikiano huo choroko linaweza kuwa zao la kimkakati lenye mchango mkubwa katika uchumi wa Taifa na ustawi wa wananchi.

Akizungumza katika mkutano wa wadau wa zao la choroko uliofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Nyerere Gold Crest, Mhe. Mtanda amesema Serikali kupitia Taasisi na Mamlaka zake imeweka mfumo imara wa uzalishaji, ukusanyaji, uhifadhi, uuzaji na malipo ya mazao kwa kutumia stakabadhi za ghala na minada ya kidijitali ili kuhakikisha soko la uhakika na bei imara kwa wakulima.

Aidha, amewahimiza Wakuu wa Mikoa kusimamia kikamilifu utekelezaji wa sera, sheria na miongozo ya Serikali, kuhamasisha wakulima kujiunga na vyama vya ushirika, pamoja na kuweka mazingira wezeshi kwa uwekezaji katika uhifadhi, usindikaji na biashara ya choroko.

Kwa upande wa wakulima, Mkuu wa Mkoa amewahimiza kutumia mbegu bora na kufuata kanuni bora za kilimo, kuvuna kwa wakati, kuzingatia taratibu za ukaushaji na uhifadhi, kuuza kupitia mifumo rasmi ya masoko, na kushirikiana na maafisa ugani pamoja na vyama vya ushirika ili kutatua changamoto za uzalishaji na masoko.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Nafaka na Mazao Mchanganyiko (COPRA), Bi. Irene Mlola amesema ushirikiano wa wadau umeleta mafanikio makubwa ambapo Tanzania imeanza kutambulika kimataifa kama nchi inayothamini wakulima wake, kuwasajili katika mifumo rasmi na kuongeza tija kuanzia uzalishaji hadi sokoni.

Bi. Mlola amebainisha kuwa katika msimu wa mauzo ya choroko wa mwaka 2025, jumla ya tani milioni 23.4 ziliuzwa kupitia minada na mifumo rasmi, na kuingiza zaidi ya shilingi bilioni 28.9.

Ameongeza kuwa Mamlaka imeendelea kutoa miongozo, mafunzo kwa maafisa ugani na kuhamasisha uwekezaji, huku mikoa ya Simiyu, Mwanza na Shinyanga ikiongoza kwa uzalishaji na mauzo katika mfumo rasmi.

Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Mkoa wa Mwanza, 2 Regional Drive
S.L.P: 119, Mwanza.
Simu: 028-2501037
Simu ya Mkononi: 028-2501037
Barua Pepe: ras@mwanza.go.tz
Hakimiliki©2018. Mkoa wa Mwanza . Haki zote zimehifadhiwa.