RAS BALANDYA ATOA MAAGIZO KWA BARAZA LA MADIWANI UKEREWE USIMAMIZI WA HALMASHAURI
Katibu Tawala Mkoa wa Mwanza Ndugu Balandya Elikana ametoa maagizo kadhaa kwa baraza la Madiwani Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe ikiwemo kusimamia Halmashauri hiyo kwa uzalendo ili kuwasaidia wananchi hususan kwenye matumizi ya fedha za umma.
Ametoa maagizo hayo mapema leo juni 17, 2025 kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa katika Baraza Maalum la kupitia hoja na taarifa ya utekelezaji wa mapendekezo ya mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali kwa halmashauri ya wilaya hiyo kwa mwaka 2023/24 lililofanyika kwenye ukumbi wa halmashauri hiyo mjini Nansio.
Aidha, Ndugu Balandya ameitaka Halmashauri hiyo kuendelea kujibu hoja za Mkaguzi na kuendelea kushirikiana na Ofisi hiyo kwa kuwa Halmashauri inaye Mkaguzi wa ndani hivyo amewataka kumtumia Mkaguzi huyo ili aisaidie Halmashauri kuweza kujifahamu hali zao kabla Mkaguzi wa nje hajafika.
Kuhusu hoja ya utumiaji usioridhisha wa mfumo wa usimamizi wa mali za serikali (GAMIS), Katibu Tawala ameagiza halmashauri hiyo ndani ya kipindi cha robo ya kwanza kutumia wataalamu kutoka Sekretarieti ya Mkoa kuwajengea uwezo wataalam wa ugavi ndani ya halmashauri hiyo ili kumaliza tatizo.
Mkuu wa wilaya hiyo Mhe. Christopher Ndubiagai ametumia baraza hilo kuwakumbusha wajumbe wa baraza hilo kusimamia makusanyo na matumizi ya fedha za umma kwa masilahi ya wananchi wa Ukerewe na akawaalika kushiriki ziara ya Mhe. Rais atakayoifanya juni 19-21 Mkoani humo.
Kaimu Mkaguzi Mkuu wa Nje Mkoa wa Mwanza ndugu Henry Chausa amebainisha kuwa kwa mwaka wa 2023/24 halmashauri ya wilaya ya Ukerewe ilifanyiwa ukaguzi kwa hesabu na kupata hati inayoridhisha na kwa miaka mitatu mfululizo imeendelea kupata hati inayoridhisha.
"Hoja za miaka ya nyuma halmashauri ilikua na mapendekezo 18 na baada ya uhakiki 16 zipo kwenye hatua za utekelezaji na 2 bado hazijafanyiwa kazi pamoja na agizo 1 la LAAC kutokana na kukosekana na kukosa vielelezo na mkakati wa CMT kujibu hoja." Amesema Chausa.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Mkoa wa Mwanza, 2 Regional Drive
S.L.P: 119, Mwanza.
Simu: 028-2501037
Simu ya Mkononi: 028-2501037
Barua Pepe: ras@mwanza.go.tz
Hakimiliki©2018. Mkoa wa Mwanza . Haki zote zimehifadhiwa.