RAS BALANDYA ATAKA MIRADI YA MAENDELEO KUKAMILIKA KWA WAKATI
Katibu Tawala Mkoa wa Mwanza Ndugu Balandya Elikana ameziagiza Halmashauri za Mkoa huo kuweka utaratibu wa kutenga fedha na kupeleka kwenye miradi ya maendeleo ili ikamilike na huduma ziweze kutolewa kwa jamii.
Katibu tawala ametoa maagizo hayo leo tarehe 17 juni, 2025 wilayani Kwimba kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wakati akiongoza baraza maalum la hoja za mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali kwa halmashauri hiyo katika mwaka wa fedha unaoishia juni 30, 2024
Balandya amesema ukamilishaji wa miradi unasaidia pia kuokoa fedha ambazo zimewekezwa kwenye uanzishwaji hivyo si vema kutokamilisha ujenzi mathalani wa shule Nyamilama (401 M) ambao halmashauri imepeleka 205 pekee kwani ni sawa na kutupa fedha.
Vilevile, ametumia baraza hilo kuwakumbusha kuwa ni matakwa ya kisheria yanayotaka kupelekwa kwa fedha asilimia 40 ya mapato yote yanayokusanywa kutoka kasma ya mapato ya ndani.
Naye, Mkuu wa Wilaya hiyo Mhe. Ng'wilabuzu Ludigija ameliasa baraza hilo kujenga tabia ya kufanyia kazi hoja za CAG zinapoibuliwa kwa kuwasilisha nyaraka zinazohitajika kisheria kama vile viambatisho na ushahidi wa manunuzi ili kujenga halmashauri hiyo kwa pamoja.
"Watendaji wenzangu kila mmoja wetu akatimize wajibu wake, tukashirikiane kwenye kazi zetu kila siku ili kuijenga halmashauri yetu kwahiyo daima tuwe wamoja na nawatakia kila la kheri kwenye uchaguzi", amesema Balandya.
Akitoa taarifa ya ukaguzi, Kaimu Mkaguzi Mkuu wa Nje Mkoa wa Mwanza ndugu Henry Chausa amebainisha kuwa halmashauri hiyo ilifanyiwa ukaguzi kwa mwaka unaoishia juni 2024 na kupata hati inayoridhisha na kwamba kwa miaka mitatu mfululizo imepata hati hiyo.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Mkoa wa Mwanza, 2 Regional Drive
S.L.P: 119, Mwanza.
Simu: 028-2501037
Simu ya Mkononi: 028-2501037
Barua Pepe: ras@mwanza.go.tz
Hakimiliki©2018. Mkoa wa Mwanza . Haki zote zimehifadhiwa.