Kamati ya amani Mwanza Yatoa Tamko kuelekea Uchaguzi Mkuu
Kamati ya Amani ya viongozi wa dini mkoani Mwanza imeitaka Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kutenda haki kuelekea uchaguzi mkuu unao tarajiwa kufanyika Jumatano tarehe 28 octoba 2020.

Kauli hiyo imetolewa na Mwenyekiti mwenza wa kamati hiyo, Askofu Dkt Charles Sekelwa alipo kuwa akitoa tamko la viongozi wenzake kwa waandishi wa habari leo jijini mwanza.

“Tume ya Taifa ya Uchaguzi itende haki kwa vyama na wagombea wote. Ihakikishe vituo vyote vya kupiga kura vinafunguliwa mapema na huku vituo hivyo vikiwa na vifaa vyote vinavyohitajika bila kusahau mahitaji ya watu wenye uhitaji maalum”, alisema Askofu Sekelwa.

Kamati hiyo pia imewaomba wagombea na wananchi wote kukubali matokeo kwani katika ushindani ni lazima apatikane mshinda na atakayeshindwa, na hii kuepusha vurugu zitakazo pelekea uvunjifu wa Amani.

“Amani ikitoweka itaathiri watu wote bila kujali aliyeianzisha, aliyehamasisha na atakayeivunja kwani hakutakuwa na shughuli zozote kiuchumi zitakazoweza kufanyika,biashara hazitafanyika, shule, hospital hakuendeki, usafiri hautokuwepo kwani vituo vya mafuta havitafanya kazi”, Aliongeza.

Naye Sheikh Mkuu wa mkoa wa Mwanza, Sheikh Hassan Kabeke akizungumza katika mkutano huo amewataka wazazi wakae na vijana wao na kuwaelezea umuhimu wa amani na kujizuia kuingia katika mambo yoyote yanayoweza kuleta vurugu na kupelekea uvunjifu wa amani.