RC MTANDA AWAONGOZA WANANCHI WA MWANZA KUPIGA KURA
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. Said Mtanda mapema leo Oktoba 29, 2025 asubuhi amepiga kura katika kituo cha Isamilo Kaskazini B genge la Washashi na kuwaongoza wananchi wa mkoa huo kutimiza haki yao ya kikatiba ya kuchagua viongozi.

Akiongea baada ya kupiga kura Mhe. Mtanda ametoa wito kwa wananchi kujitokeza kupiga kura ili waweze kuwachagua viongozi watakaowaongoza kwa kipindi cha miaka mitano kwani hali ya usalama ni shwari sana ulinzi umeimarishwa na jeshi hilo.

Amesema kwa mkoa huo kuna jumla ya vituo 5929 na kwamba kote kuko salama na shwari kabisa na shughuli zinaendelea kama kawaida kwani serikali kupitia jeshi la polisi imewahakikishia wananchi usalama wa kutosha kwa kuweka askari wa kusimamia hilo kwa jamii.

Bi. Anna Bachuba ambaye ni mlemavu wa macho ameipongeza serikali kwa kuweka vifaa maalumu (Alama nundu) vya kuwasaidia kupiga kura walemavu bila usaidizi kama miaka ya nyuma na ametoa rai kwa wananchi wengine kufika kwenye vituo kupiga kura kwani hakuna usumbufu wowote.
