TIMU YA WATAFITI KUTOKA NSSF WAZURU OFISI YA RC MWANZA
TIMU YA WATAFITI KUTOKA NSSF WAZURU OFISI YA RC MWANZA
Leo Aprili 14, 2025 timu ya watafiti wanaoshughulikia mapendekezo ya kuongeza wigo wa huduma za hifadhi ya jamii kwa wananchi (NSSF) wamemtembelea Ofisini kwake Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. Said Mtanda kwa lengo la kujitambulisha na kikao kifupi.

Kwa kutambua umuhimu wa hifadhi ya jamii kwa wananchi, Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu-Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu aliunda kamati maalum inayoshughulikia mapendekezo ya kuongeza wigo wa huduma za hifadhi ya jamii zinazotolewa na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii ili kuhakikisha kuwa Wananchi wote wanapata kinga ya mfuko huo

Hivyo timu hiyo ya wataalamu wa Hifadhi ya Jamii wameteuliwa kufanya utafiti utakaohusisha kufanya mahojiano pamoja na kukusanya maoni kwa wananchi waliojiajiri katika shughuli za kiuchumi kwenye Mkoa wa Mwanza, Wilaya ya Nyamagana, Ilemela na Sengerema kuanzia tarehe 14 -16 Aprili, 2025.

Sambamba na hayo, wataalamu hao wameomba kupewa ushirikiano wa dhati wakati wa zoezi husika ili kupata matokeo yanayotarajiwa.

Naye, Mkuu wa Mkoa Mhe. Said Mtanda ameiahidi timu hiyo ushirikiano wa kutosha na kuwataka kutosita kuwasiliana nae pindi watakapokutana na kikwazo cha aina yoyote ili kufanikisha adhma ya Serikali.
