TANROADS watakiwa kufanya matengenezo ya Barabara kwa wakati
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhe. Mhandisi Robert Gabriel ametoa rai kwa wakala wa Barabara nchini kufanya matengenezo ya Barabara kwa wakati mara tu zinapopata changamoto ili kuwaepusha na ajali watumiaji zinazoweza kusababishwa na ubovu.

Ametoa wito huo leo wakati akifunga Warsha ya Wakala wa Barabara Nchini (TANROADS) waliyokutana mahsusi kuweka mikakati ya kukabiliana na athari za mabadiliko ya Tabia nchi kwenye Miundombinu ya Barabara iliyoratibiwa na Bodi ya Mfuko wa barabara nchini.

Vilevile, Mkuu wa Mkoa ametumia fursa hiyo kuwaalika wageni kutembelea hifadhi za Taifa zilizopo Mkoani Mwanza kama Saanane na vivutio vingine vya utalii kwa ajili ya kujionea wanyama na viumbe hai wengine pamoja na kupumzika.

"Nawapongeza Wahandisi wote wanaotambulika na natoa wito kwao kuendelea kuwa waaminifu na wazalendo wakati wakiendelea kutekeleza majukumu ya ujenzi wa Miundombinu ya Barabara kwa maslahi mapana ya nchi." amesema.

Pamoja na Mambo mengine, warsha hiyo imeenda sambamba na uzinduzi wa mfumo wa kielektroniki wa ufuatiliaji wa hali ya barabara, teknolojia ambayo ni ya kisasa inayosaidia kugundua kwa wakati matatizo ya Barabara na kuweza kuzirekebisha kwa wakati.