RC MTANDA ATOA MWEZI MMOJA KWA TAKUKURU KUICHUNGUZA KAMPUNI YA UJENZI MISUNGWI
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. Said Mtanda ametoa muda wa mwezi kwa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kuingia kazini kuichunguza Kampuni ya UJENZI MISUNGWI inayomilikiwa na Halmashauri kwa kushindwa kuandaa Taarifa yake hali iliyopelekea kuzalishwa kwa hoja na miradi kushindwa kutekelezwa.
Mhe. Mtanda ametoa tamko hilo mapema leo wakati akizungumza katika Baraza la Madiwani kuhusu hoja za Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) katika Halmashauri ya Wilaya ya Misungwi na kuwataka TAKUKURU kuharakisha uchunguzi huo ili hatua stahiki ziweze kufuatwa.
Sambamba na hilo, Mkuu wa Mkoa pia ameagiza kurudishwa kwa shilingi milioni 46 zilizotolewa kama mkopo kupitia kundi la Vijana, Aidha ametoa tahadhari kuwa wale wote waliochukua fedha hizo wazirudishe kwa wakati na hatua za kisheria zitachukuliwa kwa wale watakaoshindwa kufanya marejesho ya fedha hizo.
Kadhalika, Mkuu wa Mkoa ametoa rai kwa wawekezaji waliopatiwa viwanja na Halmashauri ambao wameshindwa kuviendeleza viwanja hivyo kuvirudisha mara moja katika umiliki wa Halmashauri ili wapewe wenye uwezo wa kuvuendeleza.
Zaidi ya hayo, Mkuu wa Mkoa ameitaka Halmashauri hiyo kufanya kazi kwa ushirikiano kati ya Wataalamu na Baraza la Madiwani ili kutokuzalisha hoja za ukaguzi.
Akiwasilisha Taarifa yake, Mwekahazina wa Halmashauri ya Wilaya ya Misungwi CPA Andrew Ndaba amesema katika kipindi cha Mwaka wa fedha 2023/2024, Hesabu za Halmashauri ya Wilaya ya Misungwi zilikaguliwa na Ofisi ya Mdhubiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, na taarifa ya ukaguzi imebainisha kuwa Halmashauri ya wilaya ya Misungwi ilipata hati inayoridhisha (Unqualified Opinion).
Halmashauri ya Wilaya ya Misungwi ilikuwa na Jumla ya Hoja 41. Kati ya hizo hoja za miaka ya nyuma zilikuwa 14 na hoja za mwaka wa fedha 2023/2024 zilikuwa 36, zilizofungwa baada ya uhakiki ni 12 hivyo hoja zilizobaki hadi sasa ni 17. Amesema CPA Ndaba.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Mkoa wa Mwanza, 2 Regional Drive
S.L.P: 119, Mwanza.
Simu: 028-2501037
Simu ya Mkononi: 028-2501037
Barua Pepe: ras@mwanza.go.tz
Hakimiliki©2018. Mkoa wa Mwanza . Haki zote zimehifadhiwa.