Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Mwanza anayesimamia Utawala na Rasilimali Watu Bw. Daniel Machunda ameitaka jamii kutumia michezo kama nyenzo muhimu ya maendeleo kwani inaweza kuwa suluhisho la changamoto ya ajira kwa vijana endapo wataweka mkazo na kusimamia kwa umakini.

Bw. Machunda amesema hayo leo Februari 19, 2026 wakatj akifungua kikao kazi kilicho wakutanisha kamati ya michezo ya Mkoa na baraza la mochezo (BMT) ambapo amesisitiza umuhimu wa kutumia kikamilifu rasilimali zilizopo mkoani humo ikiwemo Ziwa Victoria ili kuendeleza mchezo wa uogeleaji.

Amesema mazingira ya Mwanza yanatoa fursa adhimu ya kukuza vipaji vya kuogelea na kuandaa wanamichezo wenye ushindani kwa ngazi za kitaifa na kimataifa huku akisisitiza kuwa Kanda ya Ziwa ni miongoni mwa maeneo yanayoongoza kwa matumizi ya baskeli nchini hivyo ni wakati muafaka kwa vijana kutumia fursa hiyo kuinua vipato vyao kupitia mashindano na shughuli za michezo.

“Tuna mkakati madhubuti msimu huu kuhakikisha timu yetu ya mpira wa miguu inayoshiriki ligi Kuu inashika nafasi za juu katika msimu huu ili iweze kushiriki michuano ya kimataifa ngazi ya vilabu msimu ujao”. Amesema Bw. Machunda.

Naye Afisa michezo mwandamizi wa Baraza la Michezo la Taifa (BMC) Ndg. Charles Maguzu ameupongeza Mkoa wa Mwanza kwa kuwa na vyama vingi vya michezo vinavyoshirikiana kwa karibu na uongozi wa mkoa hali inayochangia mkoa huo kufanya vizuri katika baadhi ya michezo kitaifa, hususan katika ngazi ya mikoa.

“ushirikiano huo ni mfano bora wa kuigwa na mikoa mingine katika kuendeleza sekta ya michezo nchini”. Amesema Bw. Maguzu.

Viongozi hao waandamizi wa BMT wapo katika ziara fupi kwenye baadhi ya mikoa ya Kanda ya Ziwa kwa lengo la kuhamasisha michezo, kusajili vyama vya michezo na kuendeleza sekta hiyo kwa ujumla.

Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Mkoa wa Mwanza, 2 Regional Drive
S.L.P: 119, Mwanza.
Simu: 028-2501037
Simu ya Mkononi: 028-2501037
Barua Pepe: ras@mwanza.go.tz
Hakimiliki©2018. Mkoa wa Mwanza . Haki zote zimehifadhiwa.