Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. Said Mtanda ameagiza kwamba miradi yote inayotekelezwa katika sekta ya elimu msingi, iwe imekamilika ifikapo Machi 28, 2026.

Agizo hilo amelitoa leo Februari 09, 2025 alipokuwa akikagua ujenzi wa shule mpya ya Msingi ya Bukanda, iliyopo Kata ya Bukanda, Wilaya ya Ukerewe.

Mhe. Mtanda amesema kuwa serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan imetoa zaidi ya shilingi bilioni 2.5 kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya elimu katika Wilaya ya Ukerewe, ambapo miradi hiyo inaendelea kutekelezwa katika sehemu mbalimbali za wilaya hiyo.

“Serikali imewekeza kiasi kikubwa cha fedha katika sekta ya elimu msingi, na ni muhimu miradi hii ikamilike kwa wakati ili wananchi wa maeneo haya wafaidike na huduma bora za elimu,” amesema Mhe. Mtanda.

Ametoa wito kwa Halmashauri zote za Mkoa wa Mwanza kuhakikisha utekelezaji wa miradi hii unakamilika kama ilivyopangwa, akiwataka Wakurugenzi Watendaji, Wakuu wa Idara, Watendaji wa Kata, na Watendaji wa Vijiji kushirikiana kwa karibu ili kuhakikisha utekelezaji wa miradi hiyo unafanikiwa.

Aidha, Mhe. Mtanda ameeleza kuwa serikali pia imetoa shilingi milioni 201 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya sekta ya elimu sekondari katika Wilaya hiyo, ambapo amesisitiza kuwa usimamizi wa miradi hiyo inapaswa kuwa wa kiwango cha juu.

“Hatutaki kuona miradi hii ikiishia nusu. Tutasimamia kwa karibu na nitaita mkutano mkoani kujadili na kutathmini utekelezaji wa miradi hii. Hakuna kubweteka,” ameongeza.

Katika hatua nyingine, Mhe. Mtanda ametoa pongezi kwa wananchi wa Wilaya ya Ukerewe kwa kuitikia wito wa uandikishaji wanafunzi, akibainisha kuwa kiwango cha uandikishaji kimepanda kwa kiasi kikubwa. Kwa Darasa la Awali, kiwango cha uandikishaji kimefikia 105%, Darasa la Kwanza 94%, na Kidato cha Kwanza 85%.

Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Mkoa wa Mwanza, 2 Regional Drive
S.L.P: 119, Mwanza.
Simu: 028-2501037
Simu ya Mkononi: 028-2501037
Barua Pepe: ras@mwanza.go.tz
Hakimiliki©2018. Mkoa wa Mwanza . Haki zote zimehifadhiwa.