Katibu Tawala Mkoa wa Mwanza Bw. Balandya Elikana amewataka wadau wa mazingira pamoja na wananchi kuhakikisha wanavitunza na kuvilinda vyanzo vyote vya maji hususani vile vinavyopeleka maji katika Ziwa Victoria

Amesema hayo leo, Februari 11, 2026 wakati akifungua kikao kazi cha kamati ya kudhibiti taka na usafi wa mazingira kilichofanyika katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza ambapo amebainisha kuwa mazingira safi ni msingi muhimu wa kuboresha afya ya jamii na kuchochea maendeleo ya kiuchumi.

“Usafi wa mazingira ni jambo la msingi sana kwetu sote kwani unachangia afya, ustawi wa kijamii pamoja na maendeleo ya kiuchumi,” amesema Bw. Balandya.

Bw. Balandya amewasisitiza wananchi wa Mkoa huo kuepuka uchafuzi wa mazingira na utupaji holela wa taka katika maeneo ya biashara na makazi yanayowazunguka kwakuwa juhudi hizo zitasaidia kujenga jamii bora kwa sasa na kwa vizazi vijavyo.

Aidha, amewataka washiriki wa kikao hicho kujadili na kutambua mbinu bora ambazo zitasaidia kujenga jamii yenye mazingira ambayo ni safi yatakayoweza kupambana na magonjwa ya mlipuko ambayo yanaonekana kuwa ni tatizo katika jamii nyingi.

“Kikao hiki kitusaidie kutambua kuwa jamii bora hujengwa na mazingira safi kiafya na kijamii, ili kuepuka changamoto za magonjwa ya mlipuko kama kipindupindu, malaria na homa ya manjano yatupasa kutunza mazingira, Tukitunza mazingira tunaweza kujikinga na magonjwa hayo.” Amesema Bw. Balandya.

Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Mkoa wa Mwanza, 2 Regional Drive
S.L.P: 119, Mwanza.
Simu: 028-2501037
Simu ya Mkononi: 028-2501037
Barua Pepe: ras@mwanza.go.tz
Hakimiliki©2018. Mkoa wa Mwanza . Haki zote zimehifadhiwa.