Kaimu Katibu Tawala Msaidizi Mkoa wa Mwanza anaesimamia Uchumi na Uzalishaji Bi. Candidah Kyamani leo Februari 10, 2026 amefungua mafunzo maalumu yaliyowakutanisha wauzaji na wakaguzi wa pembejeo za kilimo, mifugo na uvuvi kutoka Halmashauri za Mkoa huo yaliyofanyika katika Ukumbi wa Nyakahoja.

Akifungua mafunzo hayo Bi. Kyamani amewasihi wadau hao wa kilimo kuweka mbinu madhubuti hususani matumizi sahihi ya pembejeo zenye ubora pamoja na ushirikiano ili kuongeza tija katika sekta ya hiyo ambayo ni mhimili mkuu wa uchumi wa Taifa na ustawi wa wananchi.

Amesema, kilimo ni uti wa mgongo wa uchumi wa Taifa kwani kinachangia takribani 30% ya pato la Taifa huku 60% malighafi zote za viwanda zikitoka kwenye sekta hiyo na inalihakikishia taifa usalama wa chakula kwa 100%.

Ameongeza kuwa kufanya kazi kwa pamoja kutaimarisha umoja na mshikamano, kuwezesha upangaji mzuri wa mikakati ya maendeleo na kuimarisha mnyororo wa thamani wa uzalishaji wa mazao kuanzia uzalishaji, uhifadhi hadi usindikaji, hatua itakayochochea ukuaji wa sekta ya kilimo na uchumi wa jamii kwa ujumla.

Aidha, Bi. Kyamani amewataka washiriki wa mafunzo hayo kutumia fursa hiyo kuhuisha na kuimarisha Chama cha Wauzaji wa Pembejeo Tanzania (TANADA) ili kiwe chombo imara cha kuwasaidia wakulima na kushirikiana na Serikali katika kutekeleza sera za kilimo.

Kwa upande wake Afisa Kilimo Mkuu kutoka Wizara ya Kilimo, Bi. Justa Katunzi amesema kuwa Serikali imeendelea kuimarisha mnyororo wa thamani wa upatikanaji wa mbegu bora kwa kuziwezesha taasisi za uzalishaji wa mbegu ikiwemo TARI, ASA na TOSCI kwa lengo la kuhakikisha wakulima wanapata mbegu zenye tija na faida kiuchumi.

Vile vile, Bi. Katunzi amewahimiza wadau wa mbegu chini ya Chama cha Wauzaji wa Pembejeo Tanzania (TANADA) kuhakikisha pembejeo bora zinawafikia wakulima walioko vijijini kwa wakati ili kuongeza uzalishaji, kuboresha kipato cha wakulima na kuchangia maendeleo ya Taifa.

Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Mkoa wa Mwanza, 2 Regional Drive
S.L.P: 119, Mwanza.
Simu: 028-2501037
Simu ya Mkononi: 028-2501037
Barua Pepe: ras@mwanza.go.tz
Hakimiliki©2018. Mkoa wa Mwanza . Haki zote zimehifadhiwa.