BARAZA LA RAIS LA USHAURI WA KILIMO NA CHAKULA LAKUTANA NA WADAU WA KILIMO KANDA YA ZIWA
Baraza la Kumshauri Mhe. Rais kuhusu masuala ya Chakula na Kilimo limekutana tarehe 03 Juni 2025 katika Ukumbi wa Gold Crest Hotel, Jijini Mwanza ili kujadili changamoto mbalimbali zinazokabili sekta za uzalishaji, ikiwemo Kilimo ili kuongeza tija ya uzalishaji katika mnyororo wa thamani.
Akifungua Mkutano huo Waziri Mkuu Mstaafu, Mhe. Mizengo Pinda ambaye ni Mwenyekiti wa Baraza hilo amesema Serikali imekuja na malengo makubwa sana ya kukuza uchumi na hasa imejikita katika maeneo ya uzalishaji hususani sekta ya kilimo.
Mhe. Pinda ameendelea kwa kusema ni dhahiri busara inayomuongoza Mhe. Rais inawafaa wote kwa kushiriki vyema katika kuchangia mawazo kwenye masuala ya kilimo na chakula na kuona namna ya kutumia maarifa tuliyonayo kuongeza tija katika masuala ya chakula na kilimo.
“kulingana na mnyororo wa thamani, kila zao lazima lipewe thamani kuanzia shambani mpaka sokoni”.
Aidha, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhe. Said Mtanda amewakaribisha wageni wote waliotoka nje ya Mkoa wa Mwanza na kuwahakikishia usalama na utulivu wakati wote watakapokuwa Mwanza, Kadhalika amewapongeza kwa kuchagua kufanya Mkutano huo katika Mkoa wa Mwanza na kusema kwa kufanya uchaguzi huo hawajafanya makosa kwani ni sehemu sahihi.
Pamoja na mambo mengine mkutano umetoa fursa kwa wadau wa kilimo na mifugo kujadili changamoto na kutoa mapendekezo kwa ajili ya kuboresha sekta hiyo.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Mkoa wa Mwanza, 2 Regional Drive
S.L.P: 119, Mwanza.
Simu: 028-2501037
Simu ya Mkononi: 028-2501037
Barua Pepe: ras@mwanza.go.tz
Hakimiliki©2018. Mkoa wa Mwanza . Haki zote zimehifadhiwa.