HISTORIA YAANDIKWA DARAJA LA J.P MAGUFULI LAFUNGULIWA RASMI
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan leo juni 19, 2025 amezindua na kufungua rasmi daraja la J.P Magufuli lenye urefu wa Kilomita tatu lililojengwa na kampuni ya China Civil Engineering Construction Corporationi (CCECC) kwa gharama ya Shilingi bilioni 718 pamoja na VAT.
Akizungumza na wananchi katika hafla ya ufunguzi iliyofanyika katika viwanja vya chuo cha ufundi Kalwande wilayani Misungwi Mhe. Rais amesema serikali imejidhatiti katika kuwaletea wananchi uhakika wa usafiri na usafirishaji na ndio maana kwa nyakati tofauti imeendelea kuboresha vivuko na hatimaye ujenzi wa daraja.
Dkt. Samia amesema, tangu aingie madarakani amehakikisha anakamilisha ndoto za hayati Rais wa awamubya tano ikiwemo kukamilisha miradi ya kimkakati ukiwemo daraja hilo na kwamba anayo furaha kufuta historia zenye huzuni za usafiri duni za wananchi kutumia muda mrefu kuvuka upande mmoja hadi mwingine na kwa sasa watu watatumia dakika 4 tu.
Aidha ametoa wito kwa jamii, wizara ya Ujenzi pamoja na vyombo vya ulinzi kulilinda daraja hilo na akawasihi wananchi kuongeza uzalishaji kwenye kilimo, ufugaji na biashara ili kuongeza tija kwenye maisha yao kwani daraja litaleta fursa ya kuimarisha biashara ya kikanda baina ya Tanzania na nchi za jirani.
Waziri wa Ujenzi Mhe. Abdallah Ulega (Mb) amemshukuru Mhe. Rais kwa kuandika historia ya upendo kwa kuendeleza ujenzi wa daraja la JP Magufuli kutoka asilimia 25 hadi 100 ikiwa ni kwa kulipa zaidi ya bilioni 450 akiwa amekuta yamefanyika malipo ya bilioni 250 tu.
Amesema kuwa daraja hilo ni alama kwa taifa na kwamba kanda ya ziwa inakwenda kuchechemka kiuchumi kwa makundi yote ya wafanya biashara na wajasiriamali kwani linafunganishwa na huduma zingine za uchukuzi kutoka mradi wa SGR kupitia kituo cha Fella kilichopo Kilomita 15 tu kutoka darajani.
Naye, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. Said Mtanda amemshukuru na Mhe. Rais kwa kuipatia Mwanza zaidi ya Trilioni 5.6 za miradi ya maendeleo (minne 4) na akabainisha kuwa daraja hilo litaongeza mchango wa Mkoa wa Mwanza kwenye pato la Taifa ambapo kwa sasa unachangia zaidi ya Trilioni 7 ambazo ni asilimia 7.2.
Aidha, amefafanua kuwa vivuko vilivyokua vikitumika kuvusha vitahamishiwa sehemu zingine kwa ajili ya kuimarisha huduma mathalani MV Misungwi kitapelekwa Kisorya na Rugezi na MV Sengerema kitawavusha wananchi wa visiwa vya Kanyala- Kasarazi wilayani Sengerema.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Mkoa wa Mwanza, 2 Regional Drive
S.L.P: 119, Mwanza.
Simu: 028-2501037
Simu ya Mkononi: 028-2501037
Barua Pepe: ras@mwanza.go.tz
Hakimiliki©2018. Mkoa wa Mwanza . Haki zote zimehifadhiwa.