RAS BALANDYA ATAKA MIKAKATI KUINUA UFAULU WA WANAFUNZI MAGU
Katibu Tawala Mkoa wa Mwanza Ndugu Balandya Elikana ameitaka Menejimenti ya halmashauri ya Magu kuja na mpango wa kufuta ufaulu wa daraja la nne na sifuri kwa wanafunzi ili kuhakikisha dhamira ya serikali ya kuboresha elimu inafikiwa kwa wanafunzi kupata daraja la kwanza.
Ndugu Balandya ametoa maagizo hayo leo tarehe 17 juni, 2025 wakati akiongoza baraza maalum la hoja za mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali kwa halmashauri hiyo kuishia juni 30, 2024 kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa na kubaini ufanisi usioridhisha kwa shule za sekondari na msingi kwa kipindi cha 2021-2023.
"Elimu ndio msingi wa mbeleni, menejimenti ya Magu tafadhali sana daraja sifuri halikubaliki kwa watoto wetu naomba tukajifunze kwenye halmashauri zingine wanafanyaje kuinua ufaulu mathalani Kwimba twendeni tuone wao wamewezaje kwani mazingira yetu hayatofautiani." Amesema Balandya.
Ameongeza kuwa wazazi na walezi wana wajibu wa kuwafundisha stadi za maisha watoto wao kama kufanya usafi wa mazingira na miili yao ili kuwafanya wawe na utayari wa kujibidiisha na kujenga tabia ya kujitegemea kwani tabia bwete husababisha hata kufeli kwenye masomo.
Aidha, amewaagiza Halmashauri ya wilaya ya Magu kuzingatia mahitaji wakati wa uagizaji wa dawa za binadamu kwa ajili ya kusambaza kwenye vituo vya kutolea huduma ili kuepusha kuisha kwa muda wa matumizi na kulazimika kuteketeza.
Amesema ni hasara kuwa na madawa ya zaidi ya milioni tano yaliyoisha muda wake na kulazimika kuteketeza kwani ni uharibifu wa rasilimali fedha na akaliagiza baraza hilo kufuatilia vibali vya kuteketeza dawa hizo ili zisilete madhara kwa watumiaji.
"Hoja zote ambazo hazijatekelezwa ziwekewe mkakati wa utekelezaji wake ili ziweze kufungwa hivyo naagiza muweke vielelezo na viambatanisho vyote ndani ya muda ili kuifanya halmashauri ibaki salama." Amesisitiza Katibu Tawala.
Naye, Kaimu Mkaguzi Mkuu wa Nje Mkoa wa Mwanza ndugu Henry Chausa amebainisha kuwa 2023/24 halmashauri hiyo ilikaguliwa na kupata hati inayoridhisha na kwamba kuna hoja 46 ambazo zinafanyiwa kazi na kufungwa.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Mkoa wa Mwanza, 2 Regional Drive
S.L.P: 119, Mwanza.
Simu: 028-2501037
Simu ya Mkononi: 028-2501037
Barua Pepe: ras@mwanza.go.tz
Hakimiliki©2018. Mkoa wa Mwanza . Haki zote zimehifadhiwa.