RC MTANDA ATOA MIEZI 2 KWA MANISPAA ILEMELA KUTENGENEZA MAGARI YASIYOTEMBEA
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. Said Mtanda ametoa siku 14 kwa Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela kuandaa taarifa sahihi, mpango kazi pamoja na gharama ya matengenezo ya magari kumi yanayosemekana kutokufanya kazi na kisha watumie muda wa siku 60 kutengeneza magari hayo.
Mhe . Mtanda ametoa tamko hilo leo juni 17, 2025 wakati akizungumza katika Baraza la Madiwani kuhusu hoja za Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) katika Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela ambapo amesema ni msimamo wake kila mahali anapofanya kazi huakikisha magari yote ya serikali yanafanya kazi.
“Ninataka magari yote ambayo yamelala yatengenezwe na ninakumbuka niliwahi kuja hapa kufanya oparesheni ya ukaguzi wa magari, sasa nitasiamamia tena”.
Aidha, Mkuu wa Mkoa ameitaka Halmashauri hiyo kuendelea kutekeleza kikamilifu maoni ya kamati ya Bunge, na kuendelea kujibu hoja za CAG ili ziendelee kupungua.
“Nitoe rai kuendelea kushirikiana na Ofisi ya CAG ili kupata ushauri wa namna ya kumaliza au kupunguza hoja”.
Akiwasilisha Taarifa, Mwekahazina wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela Bi. Mariam Mshana amesema Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela ilikuwa na Jumla ya Hoja 58, Kati ya hizo hoja za miaka ya nyuma zilikuwa 16 na hoja za mwaka wa fedha 2023/2024 zilikuwa 42, Hoja zilizofungwa baada ya uhakiki ni 42 hivyo hoja zilizobaki hadi sasa ni 16 na wanendelea na mchakato wa kuzifuta.
Akihitimisha kabla ya Mwenyekiti kufunga Mkutano, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza ameipongeza Manispaa ya Ilemela kufuatia kupata mtiririko wa Hati Safi za Ukaguzi za CAG kwa kipindi cha miaka sita (6) mfululizo kuanzia mwaka wa fedha 2018/2019 hadi 2023/2024
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Mkoa wa Mwanza, 2 Regional Drive
S.L.P: 119, Mwanza.
Simu: 028-2501037
Simu ya Mkononi: 028-2501037
Barua Pepe: ras@mwanza.go.tz
Hakimiliki©2018. Mkoa wa Mwanza . Haki zote zimehifadhiwa.